Home » » Mahakama yawahukumu waliokutwa na dhahabu ya mamilioni

Mahakama yawahukumu waliokutwa na dhahabu ya mamilioni

Unknown | Friday, January 12, 2018 | 0 comments
Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, imewahukumu kifungo cha miaka mitano jela  au kulipa faini ya  Sh6 milioni, wafanyabiashara wawili, Naushad Mohammed Suleiman (63) na Ali Makame Juma (36) baada ya kupatikana na hatia ya kusafirisha vipande saba vya madini ya dhahabu  vyenye thamani ya Sh 989.7 milioni bila kuwa na leseni.

Pia, mahakama hiyo imetaifisha dhahabu yote iliyokamatwa pamoja na mabegi mawili ya fedha mbalimbali kutoka nchi 15 duniani, walizokamatwa nazo, katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Aman Karume uliopo Zanzibar.

Hukumu hiyo imetolewa jana Alhamisi, Januari 11 na Hakimu Mkazi Mkuu, Wilbard Mashauri baada ya washtakiwa hao kukiri mashtaka yanayowakabili.
“Ili iwe fundisho kwa watu wengine, katika kosa la kwanza mahakama inawahukumu kulipa faini ya Sh.milioni 2 ama jela miaka 2, pia kosa la pili faini Sh.mil 4 ama jela miaka 3, mkishindwa mtaenda jela na kutumikia vifungo hivyo sambamba,” Alisema Hakimu Mashauri

Wafanyabiashara hao maarufu  ambao ni wakazi wa Zanzibar, walikuwa wanakabiliwa na makosa mawili, ambayo ni kula njama na  kusafirisha madini nje ya nchi kinyume cha sheria na bila kuwa na leseni kutoka mamlaka husika.

Washtakiwa wanadaiwa kukamatwa Novemba 29, 2017,  katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Aman Karume,  wakisafirisha madini hayo kwenda Dubai katika Falme za Kiarabu.
Hata hivyo, wafanyabiashara hao walilipa faini na kuepuka kifungo hicho.

Advertisement
==
Share this article :

0 comments:

Post a Comment

 
Support : Copyright © 2018. AFRICAN NEWS BLOG - All Rights Reserved
Imetengenezwa na Edwin Moshi
Inaendeshwa na AFRICAN NEWS BLOG