Home » » Asilimia 2.7 Ya Wafungwa Wanaishi na UKIMWI

Asilimia 2.7 Ya Wafungwa Wanaishi na UKIMWI

Unknown | Thursday, February 08, 2018 | 0 comments
Asiilimia  2.7 ya wafungwa na mahabusu waliopimwa virusi vya Ukimwi (VVU) kwa mwaka 2016/17 wamegundulika kuwa na virusi vya ugonjwa huo.

Matokeo hayo yamebainika baada ya Jeshi la Magereza kuwapima Ukimwi wafungwa na mahabusu 34,793. Kati yao, wanawake ni 1,451 na wanaume ni 33,342.

Akiwasilisha bungeni mjini hapa jana taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ukimwi, Makamu Mwenyekiti wa kamati hiyo, Jasmin Bunga, alisema wafungwa waliokutwa na maambukizi ni 953 (asilimia 2.7), akibainisha kuwa wanaume ni 818 na wanawake 135.

Alisema kamati yake pia ilielezwa kuwa jeshi hilo katika mwaka 2015/16 waliwapima wafungwa na mahabusu 8,287 na kati yao, waliokutwa na maambukizi ya Ukimwi ni 376, sawa na asilimia 4.5.

"Kamati ilipokea taarifa kuhusu hali ya maambukizi ya VVU magerezani pamoja na upatikanaji wa kinga na tiba ya magonjwa nyemelezi," alisema na kufafanua zaidi:

"Katika mahojiano hayo, kamati ilielezwa kuwa Jeshi la Magereza lina jukumu la kuhakikisha wafungwa na mahabusu wanapata huduma bora za afya kama ilivyo kwenye jamii nyingine."

Vilevile, alieleza kuwa kamati yake ilielezwa uwapo wa msongamano wa wafungwa na mahabusu unaoathiri huduma bora kwa wafungwa, akibainisha kuwa kwa sasa kuna wafungwa na mahabusu 39,312 wakati uwezo wa magereza ni kuhifadhi wafungwa na mahabusu 29,552.

Kutokana na hiyo, Bunga alisema kamati yake inashauri serikali itumie adhabu mbadala kwa makosa madogo kwa kuwa kufanya hivyo kutapunguza msongamano, gharama kwa serikali na uwezekano wa kuambukizana magonjwa ya homa ya ini, Ukimwi na kifua kikuu.

Alisema kamati yake pia ilitaka kutolewa elimu ya mara kwa mara ili wafungwa na mahabusu wapate uelewa namna ya kupambana na janga la Ukimwi pamoja na wapatiwe chanjo ya kuzuia ugonjwa wa homa hatari ya ini.

"Shughuli zozote zinazohusu dawa za kulevya na Ukimwi magerezani, uongozi wa magereza uwahusishe waratibu wa Ukimwi na dawa za kulevya wa mikoa na wilaya ili kubadilishana uzoefu na elimu," alisema.

Kiongozi huyo wa kamati pia alisema wamebaini kuna upungufu wa dawa aina ya Septrine ambazo ni muhimu kwa watu wanaoishi na VVU (WAVIU).

Kutokana na changamoto hiyo, alisema kamati yake inaishauri serikali kuhakikisha dawa hizo zinazotumika kupambana na magonjwa nyemelezi, zinapatikana kwa wingi na ziingizwe katika orodha ya dawa za ARVs ambazo wanapewa WAVIU ili kufubaza makali ya VVU na kuepusha magonjwa nyemelezi.

Bunga pia alisema kamati yake imebaini kampeni za mwitikio wa masuala yanayohusiana na VVU na Ukimwi ni kama zimekufa na hivyo watu sasa wanafanya ngono zembe bila hofu.

Alisema ukimya huu umesababisha watu kujisahau na hivyo kufanya ngono zembe, hali ambayo inaweza kuleta mfumuko mkubwa wa maambukizi mapya ya VVU.

"Kamati inashauri serikali kuwa na mikakati kuhakikisha kamati za kudhibiti Ukimwi katika kila ngazi zinafanya kazi ipasavyo," alisema.

Advertisement
==
Share this article :

0 comments:

Post a Comment

 
Support : Copyright © 2018. AFRICAN NEWS BLOG - All Rights Reserved
Imetengenezwa na Edwin Moshi
Inaendeshwa na AFRICAN NEWS BLOG