Home » » Yupo Hoi hospitali baada ya Kipigo cha Chokoraa aliyekataa kumpa hela ya sikukuu

Yupo Hoi hospitali baada ya Kipigo cha Chokoraa aliyekataa kumpa hela ya sikukuu

Unknown | Thursday, December 28, 2017 | 0 comments
MWANAMUME amelazwa katika hospitali moja ya Kaunti ya Kirinyaga Kenya baada ya kuviziwa na mtoto mmoja wa mtaani akimdai pesa za Sikukuu ya Krismasi kwa msingi kuwa ndiye "baba mzazi aliyekwepa majukumu ya ulezi".
Mwanamume huyo kutoka Kijiji cha Kandongu alifumaniwa katika mji wa Ngurubani mnamo Desemba 25 na alipoulizwa kuhusu pesa za sikukuu, akasema hana.

Kwa mujibu wa Kamanda wa polisi wa Mwea Mashariki, Kizito Mutoro, mwanamume huyo alitandikwa kwa kigongo kichwani, akaanguka chini nao watoto wengine wa mtaani wakaingilia na kumtandika kisawasawa wakimuonya kuhusu kuhepa majukumu ya ulezi.


Hata hivyo, mwanamume huyo aliyejitambulisha kama David Muriithi Wachira, 33, alijitetea akisema kuwa alikuwa mwaathiriwa wa utapeli wa vijana hao wa mitaani ambao mara kwa mara hutekeleza visa kama hizo dhidi ya wanaume.
“Mimi sio baba ya mtoto huyo. Sijawahi hata kuzaa nje ya ndoa yangu na nilishangaa kusikia nikidaiwa Sh10, 000 na kijana ambaye hata sijawahi kumuona,” amesema Wachira.
Amesema kuwa yeye alikuwa katika pitapita zake ambapo alisikia amesimamishwa kwa kushikwa mashati na ndipo hadithi hiyo ikaundwa papo hapo akiitishwa Sh10, 000.
“Nilishtukia tu nimezabwa kofi, kisha nikaangukiwa na kigongo kichwani, nikajihisi nikiishia na nguvu za magoti na mara ya mwisho nakumbuka tu nikianguka chini,” akasema akiwa katika hospitali ya umma ya Kimbimbi.
Babake mwathiriwa, Nahashon Wachira sasa anamtaka Kizito Mutoro awakamate vijana hao na waadhibiwe.
“Kwa sasa tunashindwa nini kinaendelea. Polisi wanalea wezi hatari wakisema kuwa hao ni chokoraa. Hawa wanaoanza na utapeli wa kiwango hiki ndio kesho watakuwa wamejihami kwa bunduki. Ni lazima hatua ichukuliwe sasa,” akasema.
Mutoro amesema kuwa maafisa wake wameagizwa watekeleze msako dhidi ya watoto hao wa mitaani.
Share this article :

0 comments:

Post a Comment

 
Support : Copyright © 2018. AFRICAN NEWS BLOG - All Rights Reserved
Imetengenezwa na Edwin Moshi
Inaendeshwa na AFRICAN NEWS BLOG