Kikao
cha wabunge wa chama tawala cha African National Congress (ANC) leo
kimepitisha uamuzi kwa kauli moja kuwasilisha hoja ya kupiga kura ya
kukosa imani dhidi ya Rais Jacob Zuma siku ya Alhamisi.
Kwa
mujibu wa watu kutoka ndani ya kikao hicho, Spika wa Bunge, Baleka
Mbete atapanga ratiba kuruhusu chama cha Economic Freedom Fighters (EFF)
kuwasilisha bungeni hoja hiyo Alhamisi mchana. Kisha hoja hiyo
itafanyiwa marekebisho na wabunge wa ANC.
Vyanzo
kutoka ANC vinasema ni Naibu Waziri wa Mawasiliano, Tandi Mahambehlala
pekee aliyejaribu kuanzisha mjadala kuhusu jambo hili, lakini alipingwa
na wabunge wenzake ambao ni wengi.
Kikao
hicho kilifanyika katikati ya mvutano mkubwa wa kisiasa ndani ya chama
chenye Serikali ambacho kimeshindwa kumshawishi Rais Zuma kuondoka
ofisini kwa hiari.
Mhasibu
Mkuu wa ANC, Paul Mashatile ndiye alihutubia kikao hicho siku ambayo
watu watatu wanaotuhumiwa katika kashfa ya kuiweka Serikali mfukoni
walikamatwa na polisi wa kitengo cha kupambana na ufisadi (Hawks).
Kikosi
hicho cha Hawks kilivamia Jumatano asubuhi makazi ya familia ya Guptas
ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakinyoshewa kidole kwa tuhuma
zinazomkabili Zuma za kuiweka Serikali mfukoni.
Awali
kikao hicho kilipangwa kufanyika saa 4:00 asubuhi, lakini kilisogezwa
hadi saa 5:00 kwa matarajio kwamba Zuma angehutubia Taifa saa nne.
Hata
hivyo, baadaye ilitolewa taarifa iliyoonyesha kwamba Zuma bado hakuwa
tayari kuutangazia umma. Kulikuwa na uvumi kwamba Zuma angeweza kutumia
fursa hiyo kujiuzulu baada ya ANC kumpa onyo la mwisho.
0 comments:
Post a Comment