Home » » Sumatra yajipanga kuruhusu mabasi kusafiri kwa saa 24

Sumatra yajipanga kuruhusu mabasi kusafiri kwa saa 24

Unknown | Monday, January 08, 2018 | 0 comments
Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Majini na Nchi Kavu (SUMATRA), imeeleza kuwa ina mpango wa kufunga mfumo wa kuratibu mwenendo wa mabasi (VTS), katika mabasi yote ili kuweza kukusanya taarifa za mwenendo wa mabasi yanayosafirisha abiria kwenda mikoa mbali mbali hapa nchini.

Mkurugenzi Mtendaji wa Sumatra, Williard Ngewe, alieleza hayo jana, Jumapili, Januari 7, 2018, jijini Mbeya wakati wa mkutano wa kutoa elimu kwa wadau wa usafirishaji mkoani humo juu ya sheria mpya ya usimamizi wa usafiri wa mabasi.

Mkurugenzi Ngewe aliongeza kuwa wameamua kufunga mfumo huo ili kupima mwenendo wa mabasi ya mikoani na kisha baadae kuruhusu mabasi hayo yawe yanafanya safari zake muda wowote (mchana na usiku) ili kuongeza tija katika sekta ya usafiri nchini.

Alisema mfumo huo unasaidia mamlaka hizo mbili kutambua matatizo kwenye mabasi pindi inapotokea na hivyo hatua za haraka kuchukuliwa ili kudhibiti madhara.

“Kuna kitufe maalumu kwenye mfumo huo ambacho dereva anapopata tatizo, ikiwamo basi kutekwa, kupata ajali ama basi linapoharibika katika sehemu ambayo inayotakiwa ulinzi, anabonyeza kisha taarifa zinafika Sumatra na Polisi…(halafu) tunachukua hatua za haraka kuokoa,” alisema Ngewe.

Aliongeza kuwa lengo kubwa la kufunga mfumo huo kwenye mabasi ya abiria yaendayo mikoani, ni katika kuhakikisha kuwa wanapunguza ajali kwa kuratibu mwenendo wa madereva, kondakta pamoja na usalama mzima wa basi  linapokuwa safarini.

Kwa upande wake, Meneja wa Huduma za Sheria wa Sumatra, Leticia Mutaki, alisema kwa mujibu wa sheria mpya ya usafirishaji, miongoni mwa makosa yaliyoainishwa kuwa yanaweza kulifungia basi ni kuchezea mfumo huo wa VTS.

Meneja Mutaki, alisema kutokana na malalamiko ya wadau na maoni mbalimbali yaliyotolewa, sheria hiyo imeshafanyiwa marekebisho na kwamba makosa ya mmiliki na dereva yametofautishwa na kila mmoja wao ana nafasi yake katika basi husika.

Alisema dereva pamoja na kondakta watawajibika kwa vitendo vyote vya utovu wa nidhamu wakati wakiendelea na safari ikiwamo kuonyesha video ambazo zipo kinyume cha maadili zikiwamo za watu wanaoonekana wakiwa watupu.

“Lengo la kuanzisha mfumo huu ni kuongeza tija kwenye sekta yetu hii ya usafirishaji, sasa sheria imeweka wazi kuwa endapo mfumo huo utabainika kuwa umechezewa, basi husika litafungiwa kufanya kazi kwa siku 30,” alisema Mutaki.

Advertisement
==
Share this article :

0 comments:

Post a Comment

 
Support : Copyright © 2018. AFRICAN NEWS BLOG - All Rights Reserved
Imetengenezwa na Edwin Moshi
Inaendeshwa na AFRICAN NEWS BLOG