Home » » Rais Magufuli apokea hati za utambulisho wa Mabalozi wa nchi sita

Rais Magufuli apokea hati za utambulisho wa Mabalozi wa nchi sita

Unknown | Monday, January 22, 2018 | 0 comments
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 22 Januari, 2018 amepokea hati za utambulisho kutoka kwa Mabalozi 6 walioteuliwa kuziwakilisha nchi zao hapa nchini.

Mabalozi waliowasilisha hati zao ni Mhe. Konstantinos Moatsos – Balozi wa Ugiriki hapa nchini mwenye makazi yake Nairobi nchini Kenya, Mhe. Fafre Camara – Balozi wa Mali hapa nchini mwenye makazi yake Addis Ababa nchini Ethiopia na Mhe. Dina Mufti Sid – Balozi wa Ethiopia hapa nchini mwenye makazi yake Nairobi nchini Kenya.

Wengine ni Mhe. Elizabeth Taylor – Balozi wa Colombia hapa nchini mwenye makazi yake Nairobi nchini Kenya, Mhe. Martin Gomez Bustillo – Balozi wa Argentina hapa nchini mwenye makazi yake Nairobi nchini Kenya na Mhe. Uriel Norman R. Garibay – Balozi wa Ufilipino mwenye makazi yake Nairobi nchini Kenya.

Mhe. Rais Magufuli amewapongeza Mabalozi wote kwa kuteuliwa kuziwakilisha nchi zao hapa nchini na ameahidi kuwapa ushirikiano utakaowezesha uhusiano na ushirikiano kati ya Tanzania na nchi zao kukua zaidi.

Mhe. Rais Magufuli amewahakikishia kuwa Tanzania inatambua uwepo wa fursa mbalimbali za kibiashara na kiuchumi katika nchi hizo pamoja na ujuzi na uzoefu katika nyanja mbalimbali, na kwamba ni matarajio yake kuwa ujio wao utasaidia kuongeza manufaa ya kiuchumi na kubadilishana uzoefu.

Pia Mhe. Rais Magufuli amewaomba Mabalozi hao kufikisha salamu zake kwa viongozi wa nchi zao na amewakaribisha kutembelea Tanzania.

Gerson Msigwa

Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU

Dar es Salaam

22 Januari, 2018

Advertisement
==
Share this article :

0 comments:

Post a Comment

 
Support : Copyright © 2018. AFRICAN NEWS BLOG - All Rights Reserved
Imetengenezwa na Edwin Moshi
Inaendeshwa na AFRICAN NEWS BLOG