Home » » Sheikh ashauri Viongozi wa dini kuacha siasa misikitini, kanisani

Sheikh ashauri Viongozi wa dini kuacha siasa misikitini, kanisani

Unknown | Saturday, December 30, 2017 | 0 comments


11D6C078-FF9F-4E11-A767-3CEE375EA215.jpeg
MWENYEKITI wa Kamati ya Amani Mkoa wa Dar es Salaam ambaye pia ni Shehe wa mkoa huo, Alhad Mussa Salum amewataka viongozi wa kidini kuacha siasa za chuki dhidi ya viongozi wa kitaifa katika majukwaa yao ya ibada.

Akizungumza Dar es Salaam jana, Shehe Alhad alisema siku za hivi karibuni kumejitokeza baadhi ya viongozi wa kidini kutoa kauli mbalimbali zenye lengo la kuwachonganisha wananchi na viongozi wakuu wa kitaifa akiwemo Rais John Magufuli, suala alilodai halina budi kukemewa kwa kuwa sio mahali pake.

Alisema viongozi wa kidini wana nafasi kubwa katika jamii na kutokana na nafasi hizo pia wanazo fursa mbalimbali za kuwasilisha mawazo yao bila tatizo lolote kwa kufuata utaratibu unaoeleweka, ila siyo kwa kusimama mbele ya waumini wao wakati wa ibada na kutoa kauli za kisiasa zinazolenga kuvuruga amani.

“Sisi viongozi wa kidini tumepewa wigo mkubwa sana wa kufikisha mawazo yetu, siyo kwamba tunakatazwa kuikosoa serikali kwa jambo lolote…hapana, hiyo ni haki yetu ila hapa ni utaratibu upi tunautumia kufikisha kile tunachokiona hakiendi sawa,” alisema Shehe Alhad.

Alisema Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Magufuli imefanya kazi nzuri na kubwa ikiwemo ya kukomesha ufisadi, rushwa, unyonyaji, nidhamu kazini, kudhibiti mapato na mengine, huku ikipiga hatua katika kuongeza kasi ya maendeleo, jambo alilosema ni vyema kama litapokewa kama sehemu ya kujivunia kwa viongozi hao na taifa kwa ujumla.

Alisema tangu serikali hiyo iingie madarakani miaka miwili iliyopita, Rais Magufuli pamoja na Makamu wake, Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, wamekuwa mstari wa mbele kutembelea makanisa mbalimbali na misikiti na kuzungumza na waumini pamoja na viongozi wao, na kuhoji iweje sasa kwa viongozi hao wanageuka tena na kuanza kuwavuruga.

“Utaratibu sahihi upo na wa nidhamu kwa viongozi wetu ndiyo pekee unaowezesha kulinda amani na utulivu kwa taifa hili, lakini siyo kwa kukosoana kwenye nia ya kuchochea waumini wachukie viongozi wao pasipo sababu, leo kiongozi wa dini anasimama na kukosoa, kesho msemaji wa serikali akisimama na kujibu mwisho wa siku linakuwa siyo jambo la busara, kikubwa ni kwa viongozi wenzangu wa dini kuwa na staha,” aliongeza.

Aidha, kuelekea kuukaribisha mwaka mpya wa 2018, Shehe Alhad amewaomba Watanzania wote pasina kujali itikadi zao za kidini, kuzidi kuliombea Taifa ili lizidi kwenda katika njia sahihi kama ambavyo dalili zimejionesha ndani ya kipindi hiki cha Sikukuu ya Krismasi na katika miaka miwili chini ya Rais Magufuli. Alisema ushirikiano baina ya wananchi na viongozi wao wa ngazi zote ndiyo jambo pekee litakalowasaidia kuvuka kutoka sehemu moja kwenda nyingine katika njia sahihi za mafanikio.
Share this article :

0 comments:

Post a Comment

 
Support : Copyright © 2018. AFRICAN NEWS BLOG - All Rights Reserved
Imetengenezwa na Edwin Moshi
Inaendeshwa na AFRICAN NEWS BLOG