Showing posts with label KITAIFA. Show all posts
Showing posts with label KITAIFA. Show all posts

Mabilioni ya JPM zimebaki siku sita

Unknown | Thursday, January 25, 2018 | 0 comments
Mabilioni  yaliyoahidiwa na Rais John Magufuli kwa wazabuni mbalimbali yanatarajiwa kuanza kutolewa kuanzia siku sita zijazo kama ilivyoahidiwa kutokana na zoezi la uhakiki kuwa kwenye hatua za mwisho.

Januari 3, mwaka huu, Rais Magufuli alisema angelipa madeni mbalimbali ya ndani yaliyohakikiwa ipasavyo kwa kutumia Sh. bilioni 200 zilizotengwa Februari.

"Uchumi unaenda vizuri sana, tuna pesa nyingi. Nimepanga kuanzia mwezi ujao (Februari), madeni ya ndani watu wanayodai; wazabuni waliosambaza chakula kwenye vyuo na shule, makandarasi na wafanyakazi kama walimu tutayalipa," alisema Rais Magufuli muda mfupi baada ya kukutana na Gavana mpya wa Benki Kuu, Florens Luoga Ikulu jijini Dar es Salaam.

"Yale madeni yote yatakayokuwa yamehakikiwa ilmradi yasiwe madeni hewa, mwezi unaokuja nitatoa bilioni 200 ziende zikalipe madeni," alisema.

Msemaji wa Wizara ya Fedha na Mipango, Ben Mwaipaja, jana alisema uhakiki unaendelea kufanyika maeneo mbalimbali, ili kujiridhisha na ukweli wa madeni hayo.

"Kwa sasa uhakiki unaendelea na kuanzia Februari agizo la Rais litatekelezwa kwa wale wote ambao wamehakikiwa na kujiridhisha na madeni yao tutaendelea kuwalipa kwa kuwa malipo ni endelevu," alifafanua Mwaipaja.

Rais Magufuli alipozungumza Ikulu alisema angeweza kutoa mapema fedha hizo, lakini ameona kuna umuhimu wa kuhakiki madeni husika na baada ya mchakato kukamilika ataruhusu zitolewe na kwenda kwa wananchi.

Aidha, Rais Magufuli alimwagiza Gavana Luoga kushirikiana na Wizara ya Fedha na Mipango ili wadai wa serikali wa ndani waweze kulipwa kama njia ya kukuza uchumi kwa kuwa Sh. bilioni 200 zitasambaa kwa wananchi.

"Nina uhakika zitawasaidia wananchi ambao walikuwa waaminifu, waliokuwa wazabuni, nitahakikisha wenye madeni ya ukweli na siyo uongo kupata fedha za kuwasaidia kufanya biashara," alisisitiza Rais Magufuli.

Tundu Lissu Atolewa Risasi Nyingine Mwilini Mwake

Unknown | Thursday, January 25, 2018 | 0 comments
Siku 35 baada ya Tundu Lissu kusema mwili wake bado una risasi moja baada ya kutolewa nyingine 15, jana mbunge huyo wa Singida Mashariki (Chadema) alisema kuwa madaktari wamemtoa kipande cha risasi kilichokuwa mwilini mwake.

Hata hivyo, mwanasheria huyo mkuu wa Chadema, ambaye alishambuliwa kwa zaidi ya risasi 30 akiwa ndani ya gari lililokuwa nje ya makazi yake mjini Dodoma Septemba 7 mwaka jana, alisema chuma hicho ni tofauti na risasi aliyonayo mwilini, ambayo alielezwa na madaktari wa Hospitali ya Nairobi, Kenya kuwa iko sehemu mbaya, lakini isipotolewa haiwezi kumdhuru.

“Leo (jana) madaktari wamenitoa kipande cha chuma katika sehemu ya makalio ambacho nilipokuwa Nairobi (Kenya) madaktari walikiona lakini kilikuwa ndani ya nyama wakashindwa kukitoa,” alisema Lissu

“Kipande hiki kilisogea na wamekitoa. Ni tofauti na ile risasi ambayo iko mwilini mwangu.”

Akieleza kiundani kuhusu hali yake, Lissu alisema anaendelea vizuri.

“Huu mkono wa kushoto ambao ulikuwa na tatizo, wameunyoosha na kuufanyia mazoezi kweli kweli na huu mguu wa kulia ambao ndio wenye tatizo, unaendelea vyema,” alisema.

“Huku ni mazoezi tu. Kwa siku nafanya mazoezi kwa saa nne, Naingia saa 3:00 asubuhi hadi saa 4:00 asubuhi, narudi tena saa 5:00 asubuhi hadi saa 6:00 mchana. Mwisho naingia mazoezini saa 8:00 mchana hadi saa 10:00 jioni. Hiyo ndiyo ratiba yangu kwa siku.”

Alisema katika mazoezi hayo anatumia magongo maalumu pamoja na kiti cha magurudumu.

“Mfano, huu mguu wa kulia natakiwa kuukanyagia kwa kilo 20 hadi 25 katika mzani na mimi nina kama kilo 90. Ninapoukanyagia ninaulizwa kama unauma, ikiwa sijasikia maumivu ina maana sijafanya kitu, kwa hiyo ni kazi kwelikweli,” alisema.

Kuhusu muda ambao anatakiwa kufanya mazoezi hayo mpaka atakaporejea katika hali yake ya kawaida, Lissu alisema bado hajajua.

“Ah bwana we, hapa madaktari wamegoma kunieleza hilo, lakini wameangalia katika maungio ya goti la mguu wa kulia kuna mfupa haujaunga vizuri, ni lini utaunga hilo sijajua,” alisema.

Mara baada ya kushambuliwa kwa risasi na watu ambao hadi sasa hawajajulikana, Lissu alipelekwa Hospitali ya Rufaa ya Dodoma kwa matibabu ya awali kabla ya kuhamishiwa Hospitali ya Nairobi nchini Kenya siku hiyo usiku.

Desemba 21 mwaka jana wakati akihojiwa na kituo cha televisheni cha Azam, Lissu alisema madaktari wa Nairobi walimueleza kuwa risasi iliyokuwa imesalia mwili haina madhara.

Alisema risasi saba zilitolewa na madaktari hao, jambo lililomaanisha kuwa risasi nyingine nane, zilitolewa na madaktari wa Tanzania, saa chache baada ya kushambuliwa alipofikishwa Hospitali ya Mkoa wa Dodoma. 
 
Support : Copyright © 2018. AFRICAN NEWS BLOG - All Rights Reserved
Imetengenezwa na Edwin Moshi
Inaendeshwa na AFRICAN NEWS BLOG